Header Ads

LightBlog

Dk. Slaa hatarini



Tishio kwa maisha ya Dk. Slaa lisipuuzwe


Na Ndimara Tegambwage



MAISHA ya Dk. Willibrod Slaa yametajwa kuwa hatarini. Chama chake kinasema kuna “mradi” wa kuzimisha maisha yake kwa kutumia sumu.



Dk. Slaa ni Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema). Mbunge kwa miaka 15. Mgombea urais mwaka 2010; na bado kuna uwezekano wa kumtuma tena mwaka huu.
Dk. Willibrod Slaa

                                                        

Kinachoshangaza wengi ni kutosikia taratibu za kupima afya ya Dk. Slaa ili kuona kama tayari amedhurika. 

Kama kuna taarifa za kutaka kumuua kwa sumu, ina maana anaweza kuwa amelishwa sumu tayari ambayo inaua taratibu.  



Tishio kwa maisha siyo jambo la kudharau. Félix-Roland Moumié wa Cameroon aliuawa kwa kula sumu aina ya thallium aliyowekewa katika chakula, mjini Geneva, Uswisi tarehe 3 Novemba 1960. Taarifa zilitaja maofisa wa Idara ya Usalama ya Ufaransa (SDECE) kuhusika na kifo hicho.

 Félix-Roland Moumié


Moumié aliauwa miaka miwili baada ya kuchukua uongozi wa chama cha kizalendo cha nchi hiyo – Union du Peuple Camerounais. Aliyekuwa kiongozi wa chama hicho, Ruben Um Nyobe aliuawa kwa njama hizohizo Septemba 1958. Ni mazingira hayahaya. 

William Bechtel anayetajwa kutumia sumu hiyo kumuua Moumié, alifahamika kuwa mwanachama wa kikundi cha kishushushu kilichoitwa Main Rouge (mkono mwekundu); kilichokuwa na jukumu la kuua wazalendo Afrika ambao walipingana na utawala uliokuwapo; na ulioungwa mkono na Ufaransa.


Alexander Litvinenko wa Urusi alifia mjini London, Uingereza, Novemba 2006, wiki tatu baada ya kulishwa sumu iitwayo  polonium-210.



Alifariki akidai kuwa kilichomkumba kwa wiki tatu za mahangaiko, kina mkono wa rais wa sasa wa Urusi, Vladimir Putin; madai ambayo yalileta tetemeko katika uhusiano wa Urusi na Uingereza.
                                                                                                                               Alexander Litvinenko
Litvinenko, aliyekuwa ofisa katika idara ya ushushushu nchini Urusi (FSB) na shrikika la kijasusi la nchi hiyo (KGB), alikimbia mashitaka katika mahakama za Urusi.

                                                                                                        

                                                                                   
Akiwa nchini Uingereza alifanya kazi katika idara za kishushushu – za MI5 kwa mambo ya ndani ya nchi; na MI6 kwa ushushushu nje ya nchi. Alikufa.



Georgi Markov wa Bulgaria alifariki tarehe 7 Septemba 1978 kutokana na sumu iitwayo ricin. Mmoja wa wapinzani wa serikali, Markov alifia mjini London alikokuwa mkimbizi.

Georgi Markov

Markov alivuka daraja la Waterloo. Akasimama kwenye kituo cha mabasi ili aende shrika la utangazaji la Uingereza, BBC. Mara akasikia mchomo kwenye paja lake la kulia. Alipogeuka alikuta mwanaume mmoja akiokota mwavuli.



Mwanaume huyo alimwambia, “Oh, samahani!” iliyosikika katika lafudhi ya kigeni na siyo ile ya London. Halafu mwanaume huyo akasimamisha teksi na kuondoka. Siku nne baadaye, Markov alifariki.



Kilichomuua Markov ni mwavuli ambao ncha yake ilikuwa na sumu. Kwa mara nyingine, Urusi ilitajwa; mara hii kwa kushirikiana na Bulgaria “kuua mpinzani.” Hata ndani au nje ya nchi, watakuwinda!


Daktari alipokata kipande cha nyama pajani ambako Markov alichomwa na kukichunguza, alikuta kitu kama kidonge chenye ukubwa wa milimita 1.52 kilichotengenezwa kwa kemikali za platinum na iridium.

Ndani ya kidonge hicho chenye matundu mawili yaliyozibwa kwa nta, ndiko ilikuwa imemwagwa sumu ipatayo moja ya tano ya milimita (1/5). 

Nta hiyo iliyeyuka kutokana na joto la mwili na kuachia sumu iitwayo ricin kumiminika mwilini mwa Markov; kushambulia tezi la limfu, kusababisha damu kuvuja mwilini; na katika siku ya nne, figo na moyo kushindwa kufanya kazi. Alikufa.
                                  


Victor Yushchenko, rais wa sasa wa Ukraine aliponea chupuchupu mwaka 2004. Alilishwa sumu aina ya dioxin. Uchunguzi katika jaribio hili la kutaka kumuua, ulianza mwaka 2007, lakini hakuna hata mshukiwa aliyewahi kufikishwa mahakamani.



Daktari wake, Mykola Korpan anasema rais anaendelea vizuri na sura yake iliyokuwa imepotea katikati ya vipele na msinyao, sasa inaanza kurejea kwa kasi. 

Mwendesha mashitaka mkuu wa Ukraine amekuwa akidai kuwa ni nchi tatu tu ambazo zinaweza kuwa zimefanya jaribio hilo, “Urusi ikiwemo.” Urusi, hata hivyo, imekuwa ikikana.

Yushchenko alilishwa sumu muda mfupi kabla ya kuchukua urais mwaka 2007, akimwondoa madarakani waziri mkuu Viktor Yanukovych aliyekuwa akidaiwa “kushinda uchaguzi kwa wizi.”



Turudi nyumbani. Madai ya kuua, kujeruhi, kupoteza na kudhuru kwa njia mbalimbali, hayawezi kupuuzwa. Hii ni kwa sababu nchi hii siyo kisiwa; na hata visiwa vinafikika na kuzama katika matendo ya kiharamia.



Ni Chadema waliokosesha Chama Cha Mapinduzi (CCM) usingizi mwaka 2010; kwani waliporomosha umaarufu wa Rais Jakaya Kikwete (wa 2005), kutoka asilimia 80.28 za kura hadi asilimia 62.83 katika uchaguzi uliopita.



Ni Chadema waliozoa, katika uchaguzi wa serikali za mitaa mwaka jana, vijiji, vitongoji na mitaa mingi kuliko wakati wowote tangu uchaguzi katika mfumo wa vyama vingi vya siasa.



Ni Chadema na UKAWA sasa ambao wameshikia bango kashfa hii na ile ambazo zimeikumba serikali ya Rais Kikwete na kujipa jukumu la kueleza wananchi na dunia nzima kuwa “watawala wamechafuka; wamechoka, wakae pembeni.”



Ni vyama vya upinzani ambavyo kila kukicha vinazuiwa kufanya mikutano na kufanya maandamano. Vinafyatuliwa risasi na mabomu ya pilipili.



Ni vyama hivi ambavyo viongozi wake maeneo ya shamba – vijijini, wanatishwa, wanawekwa rumade bila sababu za msingi; na mwaka jana wengi waliporwa fursa na haki ya kugombea nafasi mbalimbali katika uchaguzi wa serikali za mitaa.



Katika mazingira haya, huwezi kupuuzia kauli au tuhuma au madai tu kuwa kiongozi huyu au yule ameundiwa njama za kumjeruhi, kumuua au kumpoteza. Ni mazingira tete. Ni mazingira hatarishi. Ni wakati wa kujenga shaka kwa kila kitu na kila kauli.



Mazingira haya katili yanaimarishwa na kauli, kwa mfano kutoka Sauti ya Kisonge (Mwembe Kisonge) Zanzibar, kuwa wao (CCM) hawatoi “nchi kwa yeyote.”



Ni kauli zinazoimarisha utukutu katika siasa; hadi viwango vya wanasiasa wa CCM kuviambia vyama vingine vya siasa na kuvitolea kauli kama, “ikulu mtaisikia redioni!”



Hizi ni kauli za ujambazi kisiasa. Haziashirii mwafaka wa aina yoyote. Ni kufa tu. Hakuna kupona. Katika mazingira haya, tena karibu na uchaguzi mkuu, madai na tuhuma za aina yoyote ile zaweza kuwa kweli.



Nchi hizi – Tanganyika na Zanzibar, ni zetu sote. Kupata mwafaka – kwa njia ya mashindano huru na haki – kwenye sanduku la kura, ndiko kila mmoja mwenye nia safi anatafuta na angetarajiwa kutafuta.



Kuua kwa sumu au silaha, visiwe sehemu ya msamiati, vitendo, wala imani za Watanzania. Dk. Slaa awepo kama wengine. Ulingo wa siasa uwe wazi na anayetaka kushindana naye apande jukwaani tumuone: Pale!


0713 614872

ndimara@yahoo.com



Imechapishwa gazeti la MAWIO, 12 Machi 2015.

1 comment

Unknown said...

We From SEO Milanisti Introduces Its Sales Sells Herbal Products Men And Women ALL PRODUCTS FROM our clients in Down's.

pembesar penis | obat pembesar penis

parfum pemikat wanita | perangsang wanita

Powered by Blogger.