Header Ads

LightBlog

MAONI YA MFUNGWA WA MwanaHALISI


Nani anataka nini katika katiba mpya? Haya ni maoni yaliyowasilishwa na Saed Kubenea wa MwanaHALISI; gazeti lililofungiwa na serikali kwa muda usiojulikana tangu 30 Julai 2012.
                                                                         
JANA (10 Januari 2013) wenye vyombo vya habari na asasi nyingine za habari waliwasilisha kwa Tume ya Katiba Mpya, mapendekezo ya asasi zao na hata kuongeza maoni binafsi kama mwenyekiti wa mkutano wa Katiba, Prof. Mwesiga Baregu alivyoruhusu.

Saed Kubenea, Mkurugenzi Mtendaji wa Hali Halisi Publishers Limited (HHPL), wachapishaji wa magazeti ya MwanaHALISI na MISETO, aliwasilisha maoni yake. Nimeyasoma asubuhi na kuyafanya moja ya mambo muhimu niliyoona leo na yenye thamani. Naomba kuwashirikisha:

Mapendekezo: Katiba Mpya (Na Saed Kubenea)
1. Kuhusu vyombo vya Habari
KATIBA itamke kuwa vyombo vya kutunga sheria (Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Baraza la Wawakilishi, Bunge la Tanganyika au Bunge la Shirikisho; na vyovyote vile vitakavyokuwepo) visitunge:
a) Sheria inayopingana (inayokinzana), inayokwaza au kuingilia uhuru wa kuwa na maoni (kufikiri)
b) Sheria inayopingana, inayokwaza au kuingilia uhuru wa kujieleza (kutoa kauli)
c) Sheria inayopingana, inayokwaza au kuingilia uhuru wa habari (kupata habari zozote zinazohusu jamii zilizoko mikononi mwa serikali)
d) Sheria inayopingana, inayokwaza au kuingilia uhuru wa vyombo vya habari (kazi za utafutaji, ukusanyaji na usambazaji wa habari inayofanywa na waandishi wa habari na watangazaji)
e) Sheria inayopingana, inayokwaza au kuingilia uhuru wa kujumuika kwa amani (mikutano/maandamano ambavyo kihalisi ni njia za wanajamii kuwasiliana au kupeleka ujumbe kwa wahusika)

2. Kuhusu Mamlaka ya DPP
Katiba itamke kuwa:
a) Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP) ateuliwe na chombo huru cha uteuzi (siyo rais wa nchi) na athibitishwe na Bunge
b) DPP awajibike kwa Bunge (Chombo cha kutunga sheria)

3. Mapendekezo mengine
1. Katiba itamke kuwa ARDHI ni mali ya Watanzania. Isiwekwe chini ya rais bali iwe chini ya wananchi wa Tanzania. Serikali itakuwa tu na mamlaka ya kutwaa ardhi kwa ajili ya manufaa ya umma ambayo yameainishwa kama vile ujenzi wa miundombinu, utunzaji wa mazingira na uboreshaji makazi. Serikali isiwe na uwezo wa kutwaa ardhi kwa ajili ya uwekezaji wa mtu binafsi au kampuni kama inavyoelezwa sasa na Sheria ya Ardhi ya Mwaka 1999.

2. Katiba itamke kuwa kila kijiji kitakuwa na serikali ya kijiji ambayo itaongoza kijiji hicho pamoja na uwezo wa kutunga sheria ndogo na kuzipitisha chini ya usimamizi wa mkutano mkuu wa kijiji. Serikali za vijiji ndizo zitakuwa na mamlaka ya kusimamia na kulinda haki za wananchi juu ya umiliki wao wa ardhi ya kijiji na kupanga mipango ya matumizi ya ardhi. Zitakuwa na uwezo wa kutoza kodi na kuendesha miradi ya maendeleo vijijini.

3. Katiba itamke kuwa rasilimali za madini, mafuta, gesi na maliasili, ni mali ya Watanzania na ni lazima zitumike na kuvunwa kwa manufaa ya Watanzania. Serikali haitasaini mikataba bila kibali cha bunge; bali itakuwa na uwezo wa kutoa leseni za utumiwaji wake. Utoaji huo wa leseni lazima pia uwe wa wazi na ambao utaidhinishwa na Bunge.

4. Katiba itamke kwamba migogoro yote ya uwekezaji sharti isuluhishwe kwa mujibu wa sheria za Tanzania na Mahakama za Tanzania. Hili ni takwa la Kanuni ya makubaliano ya Calvo na vilevile Azimio Na. 1803 la Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa la Mwaka 1962 na Azimio Na. 3281 la 1974 la Baraza hilo juu ya Haki na Wajibu wa Mataifa juu ya Maliasili.

5. Katiba itamke kuwa rais atachaguliwa kwa kupigiwa kura na kupata zaidi ya asilimia 50 ya kura za watu wanaotakiwa kupiga kura. Yeye na serikali yake ni lazima awajibike kwa bunge na kila uteuzi anaofanya kwa nafasi za juu za uongozi, sharti uidhinishwe na bunge baada ya Bunge kuhojiana nao.
6. Katiba itamke kuwa Bunge lina madaraka na haki ya kumfuta kazi rais kwa kutowajibika au kwa kutumia madaraka yake vibaya.

7. Katiba itamke kuwa rais hatakuwa na haki au uwezo wa kulivunja bunge kwa sababu yoyote ile.

8. Katiba itamke kuwa rais hatakuwa na kinga dhidi ya mashitaka yoyote yale akiwa madarakani na baada ya kutoka madarakani. Mtu yeyote anaweza kufungua kesi dhidi yake binafsi au ofisi yake.

9. Katiba itamke kuwa uteuzi wa majaji wa mahakama kuu na mahakama ya rufaa ufanywe na chombo huru (badala ya rais) na ufuate umahiri na uelewa wa sheria pamoja na uadilifu wa kimaadili na kisheria.

10. Katiba itamke kuwa mhimili wa Mahakama, ukiongozwa na Jaji Mkuu, ndio usimamie na kuwasilisha bajeti yake bungeni (badala ya serikali kama ilivyo sasa).

11. Katiba itamke kuwa Mwenyekiti wa Tume Huru ya Uchaguzi na viongozi wengine wakuu wa tume, wateuliwe na chombo huru cha uteuzi baada ya wanaotaka nafasi hiyo kuomba na kufanyiwa usaili. Aidha, maamuzi ya tume, kwa nafasi yoyote ile ya wagombea, yaweze kupingwa na mtu yeyote mahakamani.

12. Katiba itamke kuwa kukosa uadilifu au kutumia madaraka vibaya, kama itakavyothibitishwa na chombo husika, ni kosa la jinai.

13. Katiba itamke kuwa wote wanaojipatia utajiri kwa kuhujumu uchumi au watu wanaojitajirisha kwa kutumia madaraka yao ya umma, lazima washitakiwe kwa kosa la uhaini na mali zao zote, ikiwa ni pamoja na zile za walionufaika kutokana na kosa hilo, zitaifishwe.

14. Cheo cha Makamu wa Rais kiondolewe. Kibaki cha Waziri Mkuu.

15. Katiba itamke kuwa wakuu wa mikoa, wilaya (kama ni lazima kuendelea kuwa nao) wapatikane kwa kupigiwa akura ili w3aweze kuwajibika vema katika maeneo yao. Mameya wa miji na majiji nao wachaguliwe na wananchi moja kwa moja badala ya kuchaguliwa na madiwani.

16. Katiba itamke haki ya kuishi katika mazingira safi na salama lazima.

17. Katiba itamke kuwapo haki ya kufungua kesi za kutetea katiba, haki za binadamu na utawala wa sheria bila gharama zozote zile.

18. Katiba itamke kuwa elimu na afya ni haki kwa Watanzania wote.

19. Katiba itamke haki ya starehe.


Mwisho.
  •   Picha: Joseph Warioba: Mwenyekiti Tume ya Rais ya Katiba Mpya
Top of Form

No comments

Powered by Blogger.