Header Ads

LightBlog

TATIZO LA SHERIA KUHUSU HABARI NA MAWASILIANO

SITAKI

Wasioona tatizo la Mkuchika, sheria

Na Ndimara Tegambwage

SITAKI kuwa mchoyo. Someni wanavyosema baadhi tu ya wasomaji wa uchambuzi wangu juu ya hatua ya serikali ya kufungia gazeti la KuliKoni iliyochapishwa kwenye ukurasa huu Jumapili iliyopita.

Hadi jana saa tatu asubuhi, jumla ya wasomaji 127 walikuwa wameandika ujumbe mfupi wa simu na 39 wamepiga simu. Asilimia 99.7 wanapinga serikali kwa hatua iliyochukua. Someni kwa furaha:

Naungana na mada yako leo. Mimi nilidhani wanaposikia habari mbaya zinazoliletea taifa aibu, basi ni wakati mzuri wa kufundisha jamii juu ya kuishi kwa maadili mazuri, siyo kumfungia mtoa taarifa. Hii ni aibu kwa kiongozi aliyepewa dhamana – 0712-752595.

Pole na hongera kwa kuchagua kuelimisha jamii juu ya kufungiwa kwa KuliKoni – 0717-664685.

Ni kweli. Jeshi walikanusha asubuhi ileile habari ilipotoka hata bila kufanya uchunguzi wala kuomba undani wa habari ili wafanyie kazi (usianike namba yangu).

Hongera kwa article yako. Hivi waziri (George Mkuchika, wa Habari, Utamaduni na Michezo) anajua mavazi ya watoto wa kike vyuo vikuu? Majumbani nako amefika? – 0713-243231.

Mashaka yangu ni pengine waziri hajui istlahi uchi ina maana gani; uchi kwa mujibu wa nani, tatizo picha za uchi au uchi wenyewe? Kama watembea uchi wamo katika ibada je, picha za uchi magazetini ndio kero kuu ya wananchi Tanzania? – 0713-326376.

Tatizo kuu kabisa la wanaoitwa viongozi wetu, ni UNAFIKI. Kujikataa ndiyo uswahili wenyewe na utamaduni wa taifa. Inasikitisha. Inafedhehesha. Inadharaulisha. Reason na logical thinking havipewi nafasi kuchanua. Nakuomba endelea kuandika akina Mkuchika wapungue – 0754-532797.

Dawa ya kufungia gazeti ni kumpa kibano aliyelifungia kama ilivyokuwa kwa MwanaHALISI. Mbona safari hii kama hamumwoni? Mwasubiri nini? Kazi njema – 0787- 155882.

Nimesoma uchambuzi wako. Umenifurahisha kwa kuwa umeongea ukweli – 0716-455073.

Mungu akupe nguvu na hekima zaidi. Waandishi kama wewe mnapigwa vita lakini Mungu yupo upande wetu; amekushika kwa mkono wake wa kuume; hautatetereka. Songa mbele. A luta continua – 0715-808283.

Nimekusoma. Viongozi wetu hawakai hata siku moja wakasoma magazeti na kuchambua. Magazeti yanajaribu kuwakumbusha wakuu wetu kuwa taifa maadili hakuna…lakini leo gazeti la kurekebisha uozo waziri analifungia. Kisa? Limesema mitihani imeibwa.

Tunakwenda wapi? Wanataka magazeti yaandike kibaka kaiba kuku; lakini wakiandika wakubwa wamechota mabilioni ya shilingi, huo ni uchochezi…Tunaenda kubaya sana – 0765-938181.

Nimesoma makala yao. Umenikuna. Endelea hivyo. Tutafika. Gerald wa Kyela – 0767-481431.

Ndugu mwandishi, nakuombea kwa Mwenyezi Mungu uendelee na karama yako uliopewa na Mungu. By Masunga kutoka kijiji cha Mwasayi wilayani Maswa – 0787-229774.

Una kila sababu ya kuungwa mkono. Endelea. Wewe ni mpiganaji, una kila sababu ya kuungwa mkono – 0652-411969.

Vyombo vya habari vipo kwa ajili ya kuwajulisha wananchi habari za ukweli halisi ambazo wao ni vigumu kuzipata. Je, kuna ubaya gani wananchi kujua nchi yao inaelekea wapi?

Kufungiwa kwa KuliKoni na kufutwa kwa gazeti la Leo Tena ni kuvitisha vyombo…wakubwa wameamua kuhamishia hasira zao kwa wanyonge…Mkuchika amekurupuka. Mimi kama mwananchi sikubali – 0712-703631.

Umesema magazeti kama Leo Tena huwa yanajifuta yenyewe. Tukisubiri yajifute yenyewe yatakuwa yameshaharibu sana. Nina wasiwasi kama uliliona gazeti hilo – 0755-923565.

Sijui kama hujui kama yeye (Mkuchika) ni waziri mwenye dhamana…na majukumu yake ni “kuoversee” sekta ya habari. Naamini kwa uzoefu ulionao unajua kuwa ana kila mamlaka kufanya alichokifanya kwa mujibu wa sheria. Kwamba hukubaliani na sheria hiyo hakuna ubaya ni haki yako – 0655-280400.

Sasa inabidi ianzishwe wizara ya ufisadi na utamaduni wa mikataba; pia wizara ya kufuta magazeti na vyombo vyote vya habari -0713-442524.

Nimesoma makala yako. Mbona sioni mshikamano wenu wa hadhara wa kupinga kufungiwa magazeti? Wananchi twataka mtuongoze – 0713-280002.

Nimekupata (Mkuchika na sheria yake). Zamani Bushiri alimwambia Chakubanga alipoona anaficha bagi baada ya kuona polisi: Uliyokwishavuta vitendo vyake utavificha wapi? – 0713-234722.

Naungana na wewe 100% juu ya sheria na Mkuchika hasa aya ya 28: Huwezi kutumikia umma ambao umeufunga mdomo… – 0777-722382.

Wanahabari unganeni, msiandike habari zake hadi upite uchaguzi mkuu, Oktoba 2010 – 0714-768588.

Bravo. Hapo umempasha Mkuchika. Laiti na wanahabari wengine wangekuwa na ujasiri huo (usianike namba yangu).

Wamelifungia gazeti la KuliKoni lakini lengo lao ni MwanaHALISI, RAIA Mwema na Tanzania Daima. Je, kuna uhuru wa habari – 0718-122081.

Maoni ni mengi. Kila mmoja ana lake la kusema kadri anavyoguswa. Tujiulize: Je, waziri mmoja akijiuzulu, siyo kwa kashfa za ukwapuaji mabilioni ya shilingi benki kuu, bali kwa kukataa kutumikia sheria katili, itakuwaje?

Itakuwa hivi: Serikali itakumbushwa kuwa fimbo yake, iliyoweka ili kupigia nyoka pindi akitokea, sasa inatumika kupigia mume, mke na watoto. Itupwe. Hapana. Ivunjwevunjwe na kuwa kuni. Inanyang’anya haki. Inafedhehesha.

Sheria ya Magazeti ya mwaka 1976 ni kitanzi shingoni mwa hata mawaziri wenyewe pindi watokapo kwenye “utukufu” wa wizara hiyo au wa serikali. Ina tabia ya kuwasubiri wastaafu au wastaafishwe ndipo waone kuwa ni katili kupindukia.

Kinachosikitisha ni vipi watawala wameona utamu – tangu mwaka 1976 – wa kuendelea kuwafunga midomo na akili – wazazi wao, watoto wao, ndugu zao na jamii nzima ya Tanzania.

Kuna haja kwa Watanzania kufanya maamuzi: Kama hakuchi tufungue milango – alfajiri itukute nje katikati ya maandalizi mapya ya kutafuta haki. Na wewe umo.

O713-614872
ndimara@yahoo.com
www.ndimara.blogspot.com

No comments

Powered by Blogger.